Basata yawafungia Rayvanny, Diamond Platnumz

Muktasari:

  • Wimbo Mwanza wa Rayvanny akishirikiana na Diamond Platnumz umefungiwa na Basata leo Novemba 12.

Darv es Salaam. Baraza la Sanaa Tanzania (Basata) limetangaza kuufungia wimbo mpya wa mwanamuziki Rayvanny kwa maelezo kuwa unahamasisha masuala yasiyokubalika katika jamii.

Katibu Mtendaji wa Basata, Godfrey Mngereza ameiambia Mwananchi leo Jumatatu Novemba 12,2018 kuwa wameufungia wimbo huo ambao amemshirikisha Diamond Platnumz na kupiga marufuku kuchezwa mahali popote.

Ameongeza kuwa wanawasiliana na mamlaka nyingine ili kuchukua hatua zaidi kwa kuwa tayari wimbo umeenea mitandaoni.

Kuhusu kupigwa katika tamasha lao la Wasafi linalotarajiwa kuanza kutimua vumbi Novemba 24 mwaka huu amesema nalo watalifungia iwapo watautumia.

“Tumesikitishwa sana na msanii mkubwa kama Diamond kushiriki kuimba wimbo usio na maadili kwa kuwa ni msanii mkubwa anayetazamwa kama kioo na jamii,” anasema.

Ameainisha kuwa maneno yaliyotumika katika wimbo huo yanahamasisha ngono kinyume na maumbile na matusi mengine yanayobomoa maadili.

“Nimesikitishwa sana na maneno yaliyotumika, hivi wanavyoimba hivyo hawaoni kama ndugu zao wanaweza kusikiliza wimbo huo?  Maana kutamka hadharani ni sawa na kuongea mbele ya mama yake au watoto wake,” alifanunua.