Baraka Magufuli: Sijamalizana na Rais Magufuli

Muktasari:

  • Baraka anasema angependa kufanya kazi na wasanii Steve Nyerere na Mr. JK ambao alieleza kushirikiana kwao kutawafanya kuwa na kumbukumbu nzuri ya vizazi vijavyo juu ya viongozi hao

Dar es Salaam.Mchekeshaji, Baraka Mwakipesile ‘Baraka Magufuli’ amesema anatamani kumuona kwa mara ingine Rais John Magufuli kwa kuwa bado ana mengi ya kumwambia.

Baraka zaidi ya wiki sasa amekuwa gumzo mitaandaoni baada ya kuigiza sauti ya Rais Magufuli mbele yake.

Baraka alifanya hivyo Aprili 11, 2019 baada ya kuitwa na Rais alipokuwa ziarani na kupita mjini Mafinga Wilayani Mufindi, ambako msafara wake ulisimama kwa muda ili kuongea na wananchi.

Katika mahojiano yake na Mwaspoti leo Aprili 17, 2019 alipotembelea ofisi za Mwananchi ambazo ni wazalishaji wa magazeti ya Mwananchi, Mwanaspoti na The Citizen, zilizopo Tabata Relini Jijini Dar es Salaa, Baraka alisema bado hajakinai kumuona Rais Magufuli.

Amesema siku ambayo alipita mjini Mafinga ratiba yake ilikuwa imebana sana, hivyo alipewa muda mchache wa kuonyesha kipaji chake na kueleza kwamba ana mengi ya kumuonyesha na ya kumwambia.

Akieleza namna alivyojisikia baada ya kupewa nafasi ile, alisema alifurahi kwani awali alikuwa na hofu kumuigiza mtu kama yeye.

“Yaani sasa hivi ni kama Rais kanipa uhuru zaidi kuifanya kazi hii, awali nilikuwa najiuliza huenda ingeweza kuleta shida kwa kumuigiza kiongozi mkubwa kama yeye lakini kumbe sivyo.

Katika ndoto zake za kisanaa, Baraka anasema angependa kufanya kazi na wasanii Steve Nyerere na Mr. JK ambao alieleza kushirikiana kwao kutawafanya kuwa na kumbukumbu nzuri ya vizazi vijavyo juu ya viongozi hao.