Babu Tale awatoa kimasomaso mastaa, ashinda kura za maoni CCM

Muktasari:

Wakati Mwana FA aliomba ridhaa ya wana CCM Handeni, Babu Tale yeye alikuwa aliomba ridhaa Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki.

Msanii wa Bongo Fleva, Hamis Mwinjuma 'Mwana FA' na Meneja wa msanii Diamond Platnumz, Hamis Taletale maarufu Babu Tale wamekuwa mastaa wawili wa Tanzania waliowatoa wenzao kimasomaso katika kura za maoni za Chama cha Mapinduzi (CCM).

Wakati Mwana FA aliomba ridhaa ya wana CCM Muheza, Babu Tale yeye alikuwa aliomba ridhaa Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki.

Katika kinyang'anyiro hicho Babu Tale alipata kura 318 kati ya kura 749 na kuibuka mshindi dhidi ya mshindi wa pili Omary Mgumba aliyepata kura 242 na mshindi wa tatu, Kibena Kingo aliyepata kura 40

Kwa upande wa Mwana FA yeye alipata kura 276 na kumfanya awe mshindi wa pili katika kinyang'anyiro hicho akiachwa na mshindi wa kwanza balozi Adadi Rajabu aliyepata kura 577 huku mshindi wa tatu Hassan Bomboka akipata kura 49.

Hata hivyo wakati mastaa hao waking'aa tayari wengine wao waliojitokeza wameangukia pua huku wengine wao wakikosa kura hata moja.

Kati ya hao ni Zamaradi Mketema aliyepata kura mbili, Mwijaku na Mpoki ambao wote wamepata kura sifuri.

Wengine ni Steve Nyerere aliyepata kura sita na wakili maarufu Albert Msando aliyepata kura 19.