Aurlus Mabele hatimaye azikwa

Muktasari:

Kwenye mazishi hayo yalishirikishwa wanandugu wachache wakiwamo wanafamilia pekee kutokana na sakata la ugonjwa wa corona ambao umekuwa tishio kwa sasa dunia.

MWILI wa nyota wa zamani wa kundi la Loketo, Aurlus Mabele hatimaye umehifadhiwa kwenye nyumba yake ya milele, baada ya kufariki dunia wiki iliyopita nchini Ufaransa.
Mabele aliyekuwa na umri wa miaka 66, alikumbwa na mauti Machi 20 kutokana na kukumbwa na virusi vya covid-19 zinavyosababisha ugonjwa wa corona na alizikwa jana Ijumaa nchini Ufaransa.
Kwenye mazishi hayo yalishirikishwa wanandugu wachache wakiwamo wanafamilia pekee kutokana na sakata la ugonjwa wa corona ambao umekuwa tishio kwa sasa dunia.
Mabele aliyezaliwa Congo Brazzaville, anakumbukwa kwa umahiri wake wa kutunga na kuimba akipitia makundi mbalimbali, lakini umaarufu zaidi akiwa na Loketo Group lililotamba na nyimbo mbalimbali zilizomtangaza yeye na memba wenzake akiwamo Dibla Dibala na wengine.
Kifo chake kilitangazwa na mwanae wa kike ambaye naye ni mwanamuziki, Liza Monet, ikiwa ni miaka kadhaa tangu alipokuwa akiugua kansa ya koo iliyomfanya awe nje ya fani kwa muda mrefu.