AY: Corona inatufundisha usafi

Muktasari:

Tanzania tayari ina wagonjwa zaidi ya watano waliotangazwa na Wizara ya Afya ambapo wapo chini ya uangalizi huko wengine wakiendelea kuchunguzwa.
Rafiki yake mkubwa na AY, MwanaFA naye ni miongoni wa Watanzania ambao walikumbwa na maambukizi hayo ambapo aligundulika baada ya kurejea kutoka safarini Afrika Kusini ingawa amedai anaendelea vizuri.

MKONGWE wa muziki wa kizazi kipya, Ambwene Yesaya 'AY' amesema kuingia kwa ugonjwa wa mlipuko wa virusi vya Corona nchini unawafundisha Watanzania kuzingatia suala la usafi wa mazingira kwa ujumla.
Mbali na usafi wa mazingira pia kila Mtanzania kuzingatia usafi wake binafsi kuanzia nyumbani na kwenye shughuli zake za kila siku.
Tanzania tayari ina wagonjwa zaidi ya watano waliotangazwa na Wizara ya Afya ambapo wapo chini ya uangalizi huko wengine wakiendelea kuchunguzwa.
Rafiki yake mkubwa na AY, MwanaFA naye ni miongoni wa Watanzania ambao walikumbwa na maambukizi hayo ambapo aligundulika baada ya kurejea kutoka safarini Afrika Kusini ingawa amedai anaendelea vizuri.
AY alisema kuwa; "Maambukizi ya virusi hivi tiba yake ni usafi tu, ndiyo ni janga la ulimwengu mzima ila kuingia kwake kunatufundisha ni namna gani tunapaswa kuzingatia usafi pasipo kukumbushwa.
"Jukumu la usafi linapaswa kufanywa na mtu mwenyewe ila inaonekana wengi hatuko hivyo, sasa hivi kila mtu amekuwa msafi, kila mtu ananawa kisa tu anaogopa Corona je kabla haijaingia walikuwa wanazingatia usafi huo, jibu ni hapana.
"Hakuna ugonjwa hatari kama malaria na unaua vibaya mno ila watu hawauogopi wanachoogopa sasa ni Corona ambayo kujikinga kwake ni kuzingatia usafi tu, hivyo tuendelee kujikinga kama serikali inavyotuelekeza," alisema
AY aliongeza kuwa; "Hakuna sababu ya kwenda kwenye mikusanyiko bila sababu za msingi, tubaki majumbani na mambo mengine yataendelea kufanyika kupitia mitandao ya simu,".