Mwakyembe apania Sh120 mil za ‘East Africa Got Talent' ibaki Tanzania

Muktasari:

Waziri Mwakyembe ameahidi kuhamasisha ushiriki wa shindano la East Africa Got Talent' kutoka hapa nchini ili zawadi ya Sh120 ibaki hapa nchini.

Dar es Salaam. Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Harrison Mwakyembe amesema anatamani mshindi wa ‘East Africa Got Talent' atoka Tanzania na kulamba zawadi ya Sh120 milioni ya zawadi.

Waziri Mwakyembe ameyasema hayo leo Jumatano, Aprili 10, 2019 katika uzinduzi wa shindano hilo, uliofanyika hoteli ya Serena, usaili wake hapa nchini utaanza Mei 25-26 Dar es Salaam.

Mwakyembe alisema ujio wa shindano hilo ni fursa kwa vijana wa kitanzania kwa sababu linatambulika duniani hivyo kuna kila sababu ya watanzania kujitokeza kwa wingi kushiriki ukizingatia litajumuisha vipaji mbalimbali.

Aidha amesema watalitumia katika kutangaza utalii kwani pamoja na kuwa nchi yenye mbuga za hifadhi nyingi ukilinganisha na nyingine za Afrika Mashariki, bado tupo nyuma katika uingizaji wa watalii.

Mkurugenzi wa kampuni ya Clouds Media, Joseph Kusaga  alisema wameamua kuleta shindano la nchini kama mwendelezo wa kufungua milango ya ajira kupitia burudani.

Kusaga alisema wamefarijika Clouds kuchaguliwa kuwa miongoni mwa vyombo vya habari vilivyochaguliwa kuendesha shindano hilo hapa nchini na kueleza ni kutokana na kujikita kwao katika masuala ya burudani kwa zaidi ya miaka 20 sasa.

Mchekeshaji maarufu kutoka Kenya, Anne Kansiime alisema amefurahi kuchaguliwa kuwa moja ya majaji katika shindano hilo na kueleza watu wa Afrika Mashariki sana kila sababu ya kulitumia ili kuzalisha wasanii wengine wapya.

"Tunahitaji wakina Kansiime wengi. Wakina Diamond wengine kwani na sisi itafika mahali kazi hii tutaacha," alisema Kansiime.