DULLA MAKABILA: Mapenzi yamenivuruga kimtindo

NANI asiyeufahamu muziki wa Singeli? Muziki ambao kwa sasa unazidi kujipatia umaarufu mkubwa hapa Bongo. Mbali na kuonekana kama ni wa kihuni lakini umekuwa ukipewa nafasi kubwa ya kusikilizwa na wapenzi wa muziki huo.

Muziki huu pia umewaibua wasanii wengi ambao kutokana na nyimbo zao kupendwa na mashabiki wao, wamejizolea umaarufu.

Dulla Makabila ni mmoja wa wasanii waliojizolea umaarufu kutokana na muziki huu kutokana na nyimbo zake kupendwa na mashabiki wengi zikiwamo ‘Hujaulamba’, ‘Utatoa hutoi’.

Pia Dulla ameshawahi kuwa na uhusiano wa kimapenzi na mwigizaji wa filamu Husna Sajent na hivi karibuni wametangaza kuachana bila ya kutoa sababu yeyote ya kuachana.

Mwanaspoti lilimtafuta mkali huyo ambaye kwa sasa anakutamba na kibao kipya ‘Kuingizwa’ na kupiga naye stori mbili tatu.

Mwanaspoti: Habari ya kwako Dulla?

Dulla Makabila: Nzuri dada.

Mwanaspoti: Pole sana kwa kuachwa na Husna Sajent.

Dulla Makabila: Mimi sijaachwa bali tumeachana, yeye ndio anasema ameniacha!

Mwanaspoti: Habari za mjini ndio zinadai hivyo.

Dulla Makabila: Sio kweli, wanasema tu hawajui chochote, sisi tumeachana bwana tena kwa makubaliano.

Mwanaspoti: Hivi karibuni kuna habari zilisikika ulikamatwa na Polisi baada ya kumpa ujauzito mwanafunzi na hicho ndio chanzo cha kuachana na Husna ni kweli?

Dulla Makabila: Sio kweli hizo habari, ila kuna watu wasiopenda mafanikio yangu ndiyo wanasambaza taarifa mbaya kama hizo.

Mwanaspoti: Ina maana hizi taarifa hujazisikia?

Dulla Makabila: Taarifa hizo nimezipata wakati narudi kutoka kwenye show mkoani Iringa miezi michache iliyopita, tena baada ya kupigiwa simu na meneja wa Diamond, Mkubwa Fella kuhusu habari hizo, ila hazina ukweli wowote yaani zimenishangaza sana.

Mwanaspoti: Kwa hiyo ushapata mpenzi mwingine?

Dulla Makabila: Hahaha, hakuna bado kabisa maana itanichukua muda kidogo.

Mwanaspoti: Inaekelea Husna amekuumiza eeeh?

Dulla Makabila: Ah wapi, lakini si unajua mapenzi ukiwa na malengo fulani halafu ghafla yale malengo hayajatimia basi kichwa lazima kikuvuruge.

Mwanaspoti: Inasemekana wewe una hasira sana za karibu, vipi unapokuwa na hasira cha kwanza unafanya nini?

Dulla Makabila: Mara nyingi napenda kuondoka eneo la tukio ili kuepusha shari.

Mwanaspoti: Kitu gani kimewahi kukuumiza sana maishani?

Dulla Makabila: Niliponyan’ganywa maiki na kuzomewa kwa kuonekana sijui kuimba nilipopanda jukwaani kwa mara ya kwanza.

Mwanaspoti: Umepanga kuoa ukifikia umri gani?

Dulla Makabila. Mie hata sasa hivi kwa huu umri niliokuwa nao naoa nikipata mwanamke mwenye sifa ninazotaka.

Mwanaspoti: Nashukuru sana.

Dulla: Asante karibu tena.