Wenger achekelea kumsajili kinda Mnigeria kwa bei poa

Muktasari:

Onyekuru ambaye aliitwa kwa mara ya kwanza kwenye kikosi cha Nigeria, Super Eagles mwezi huu anatarajiwa kutua Arsenal  msimu ujao wa Ligi Kuu.

Abuja, Nigeria. Baada ya Arsenal kufanikiwa kumsajili kinda wa Kinigeria, Henry Onyekuru kwa Pauni 6.8 milioni, kocha Arsene Wenger amechekelea dogo huyo kupata viza ya Uingereza.

Onyekuru ambaye aliitwa kwa mara ya kwanza kwenye kikosi cha Nigeria, Super Eagles mwezi huu anatarajiwa kutua Arsenal  msimu ujao wa Ligi Kuu.

Onyekuru, 19,  amehusishwa kwa muda mrefu na Arsenal zikieleza kuwa ofa ya Pauni 6.8 milioni imelipwa kwa klabu ya KAS Eupen ambayo imemruhusu kuichezea Arsenal msimu wa 2017/18.

Klabu ya West Ham pia ilimtaka kinda huyo baada ya kumtoa kwa mkopo kinda wao, Reece Oxford aliyeuzwa Italia.

Arsenal inayo mshambuliaji mwingine Mnigeria, Alex Iwobi  ambayealieleza kuwa Wenger amenasa kijana mwenye uwezo mkubwa kucheza soka. Vijana hao walikuwa kwenye kikosi cha Super Eagles kilichoanza vibaya kwa kufungwa na Bafana Bafana ya Afrika Kusini, mabao 2-0 kusaka tiketi ya Kombe la Afrika (Afcon) mwaka 2019.