Team Money Russia 2018

Muktasari:

Mastaa kibao unawafahamu wewe wanaotamba kwenye klabu mbali duniani, watakuwa kwenye ardhi ya Russia wakiwa na timu zao za taifa kupigania ubingwa huo wenye hadhi kubwa kabisa kwenye mchezo huo wa soka duniani.

MOSCOW, RUSSIA. MAMBO ni moto. Ile presha ya fainali za Kombe la Dunia za huko Russia imezidi kupanda huku mashabiki wa soka duniani kote wakisubiri fursa hiyo maridhawa ya kuwashuhudia mastaa wa maana wakionyesha ubabe katika fainali moja za kibabe.

Mastaa kibao unawafahamu wewe wanaotamba kwenye klabu mbali duniani, watakuwa kwenye ardhi ya Russia wakiwa na timu zao za taifa kupigania ubingwa huo wenye hadhi kubwa kabisa kwenye mchezo huo wa soka duniani.

Hebu fikiria michuano ambayo inakupa nafasi ya kuwaona wakali wote wanaotisha kwenye soka kwa sasa kuanzia kwa Lionel Messi, Cristiano Ronaldo, Neymar, Mohamed Salah, Eden Hazard, Paul Pogba, Antoine Griezmann na wengine kibao.

Kitu kingine kinachovutia fainali hizo ni kwamba zitavutia wachezaji ghali zaidi duniani, ambao wote watakwenda kuonyesha makali yao wakiongozwa na Neymar, ambaye uhamisho wake wa kutoka Barcelona kwenda Paris Saint-Germain mwaka jana uligharimu Pauni 198 milioni.

Neymar atakuwa kwenye fainali hizo kujaribu kufuta aibu ya iliyowakuta miaka minne iliyopita wakati taifa lake la Brazil lilipochapwa 7-1 na Ujerumani katika fainali ambazo zilifanyika kwenye ardhi yao. Lakini, fainali hizo za Russia hazitakuwa na wanasoka wote ghali kwa sababu kuna wengine kibao nchi zao zimeshindwa kufuzu, wakiwamo Gareth Bale na Virgil van Dijk, huku Aymeric Laporte na David Luiz wakiachwa na timu zao za Ufaransa na Brazil kwenye vile vikosi vyao vya wachezaji 23.

Mwanaspoti linakutelea Kikosi cha Kwanza cha mastaa ghali kabisa kwenye soka ambao watakuwa kwenye fainali hizo za Russia.

Kipa:

Ederson, Brazil (Benfica kwenda Man City – Pauni 35milioni)

Mabeki:

Benjamin Mendy, Ufaransa (Monaco kwenda Man City – Pauni 52milioni)

John Stones, England (Everton kwenda Man City – Pauni 48milioni)

Kyle Walker, England (Tottenham kwenda Man City – Pauni 50milioni)

Viungo:

Neymar, Brazil (Barcelona kwenda PSG – Pauni 198milioni)

Philippe Coutinho, Brazil (Liverpool kwenda Barcelona – Pauni 142milioni)

Paul Pogba, Ufaransa (Juventus kwenda Man United –Pauni 89milioni)

James Rodriguez, Colombia (Monaco kwenda Real Madrid – Pauni 63milioni)

Washambuliaji:

Kylian Mbappe, Ufaransa (Monaco kwenda PSG – Pauni 166milioni)

Cristiano Ronaldo, Ureno (Man United kwenda Real Madrid – Pauni 80milioni)

Ousmane Dembele, Ufaransa (Borussia Dortmund kwenda Barcelona – Pauni 97milioni).