Rashford huyu vipi? Atua kambini kwa bondia

Muktasari:

Rashford aliweka picha katika mtandao ikimuonesha akiwa na Joshua zikiwa zimebaki siku chache kabla ya Man United kuvaana na Liverpool Jumamosi wiki hii.

London, England. Kinda Marcus Rashford wa Manchester United amekwenda kambini kwa bondia wa ngumi za uzito wa juu Anthony Joshua.
Rashford aliweka picha katika mtandao ikimuonesha akiwa na Joshua zikiwa zimebaki siku chache kabla ya Man United kuvaana na Liverpool Jumamosi wiki hii.
Watani hao wa jadi wanatarajia kumenyana katika mchezo wa Ligi Kuu England unaotarajiwa na msisimko kutoka kwa wachezaji wa timu hizo.
Mchezaji huyo aliandika ujumbe katika mtandao huo akisema: "Ni furaha kutembelea kambi hii."
Joshua anatarajia kupanda ulingoni kuzichapa na bondia Kubrat Pulev Oktoba 28, mwaka huu mjini Cardiff na tayari tiketi 78,000 zimeuzwa.
Bondia huyo amepata umaarufu baada ya kumtwanga mbabe wa masumbwi duniani Wladimir Klitschko kwenye Uwanja wa Wembley Aprili, mwaka huu.