Kinda Mtanzania wa Ureno kujiunga na Taifa Stars mapema

Muktasari:

Taifa Stars itaingia kambini Oktoba 1, kujiandaa na mchezo wa kirafiki dhidi ya Malawi utakaochezwa Oktoba 7.

Dar es Salaam. Winga wa Kitanzania, Orgenes Mollel wa FC Famalicão ya Ureno amepanga kuwasili mapema ili kujiunga na kikosi cha timu ya Taifa Stars.
Taifa Stars itaingia kambini Oktoba 1, kujiandaa na mchezo wa kirafiki dhidi ya Malawi utakaochezwa Oktoba 7.

Hii ni awamu ya pili kwa winga huyo wa timu ya daraja la kwanza nchini humo kuitwa, awamu ya kwanza alishindwa kuwasili kutokana na taarifa zake za kiusalama kuchelewa kumfikia.

"Nina kiu kubwa ya kuichezea timu ya Taifa hivyo nitajihidi mapema kuwahi maandalizi kuelekea mchezo huo wa kirafiki, siku chache zijazo itajulikana lina nitafika, Tanzania," alisema Mollel aliyepo Ureno baada ya kufanya mazungumzo na mwandishi leo Jumapili.