Kane amnunia refa kisa England kupigwa

Muktasari:

Fowadi Kane, ambaye ndiye nahodha wa Three Lions amemshutumu mwamuzi wa kati, Danny Makkelle kwa kuwafanyia hovyo kutokana na kukataa bao lao katika dakika za mwisho kwenye mechi hiyo iliyofanyika uwanjani Wembley juzi Jumamosi usiku.

STRAIKA wa England, Harry Kane amekuwa mkali na kudai refa amechangia kuwafanya wachapwe na Hispania katika michuano mipya kabisa huko Ulaya, inayofahamika kama Uefa Nations League.

Fowadi Kane, ambaye ndiye nahodha wa Three Lions amemshutumu mwamuzi wa kati, Danny Makkelle kwa kuwafanyia hovyo kutokana na kukataa bao lao katika dakika za mwisho kwenye mechi hiyo iliyofanyika uwanjani Wembley juzi Jumamosi usiku.

Kane amemshambulia refa huyo, Makkalle aliyewahi kuwa ofisa wa polisi, kwa kukataa bao la Danny Welbeck katika dakika za majeruhi akidai kipa David De Gea alifanyiwa madhambi ndio maana aliudonoa mpira.

Kane alisema kwa hasira: “Kwenye mechi kubwa kama zile, unahitaji refa anayejielewa, si wa kuharibu mambo. Danny alikuwa amesimama tu pale, De Gea karuka juu, kadaka mpira, lakini aliposhuka chini, amemdondokea Danny.

“Danny hakwenda kumfanyia madhambi au kitu kingine chochote. Wakati mwingine makipa wanabembelezwa sana kuliko sisi wengine na bahati mbaya hili limetugharimu sisi. Nadhani tulistahili walau sare, tulicheza vizuri.”