Wenger aingia matatani England

Muktasari:

Arsenal msimu huu imeshindwa kufuzu kucheza kwa mashindano ya Ligi ya Mabingwa

London, England. Arsene Wenger anachunguzwa na Chama cha Soka England (FA) kwa kosa la kumtolea lugha ya ukali mwamuzi katika mchezo wao na Watford.
Arsenal ilichapwa mabao 2-1 na Watford katika mchezo wa Ligi Kuu England uliochezwa ambao Mfaransa huyo aliondoka uwanjani akiwa amechanganyikiwa.
Wenger alimshukia mwamuzi Neil Swarbrick akipinga baadhi ya uamuzi hatua ambayo imetafsiriwa ni utovu wa nidhamu na FA imeanza uchunguzi.
Endapo atakutwa na hatia anaweza kuchukulia hatua ikiwemo kufungiwa katika baadhi ya mechi za Ligi Kuu England.
Kocha huyo amekuwa katika mazingira magumu na mashabiki wa klabu hiyo wamekuwa wakimpigia kelele kutaka ang'oke Makao Makuu Emirates.
Mashabiki wa klabu hiyo wanamtaja Wenger ni kocha asiyetaka mabadiliko katika kikosi chake na amekuwa akiigharimu kwa kushindwa kununua wachezaji nyota.
Arsenal inashika nafasi ya sita katika msimamo wa Ligi Kuu England ikiwa na pointi 13, katika mechi nane ilizocheza msimu huu.