Batshuayi kokote kambi atua Valencia

Muktasari:

  • Mshambuliaji huyo Chelsea msimu uliopita alitolewa kwa mkopo Dortmund

London, England. Mshambuliaji wa Chelsea, Michy Batshuayi ameshindwa kurejea katika Ligi Kuu England baada ya timu zote zilizokuwa zikimuwania kumsajili kushindwa kukamilisha uhamisho huo hadi dirisha la usajili England lilipofungwa Alhamisi usiku.

Kutokana na jambo hilo mshambuliaji huyo amelazimika kujiunga na Valencia ya Hispania kwa mkopo wa muda mrefu, kumpisha Jorginho aliyetua Stamford Bridge kutoka Torino.

Batshuayi alikuwa akicheza kwa mkopo kwenye klabu ya Borussia Dortmund, msimu uliopita na kocha mpya wa Chelsea, Maurizio Sarri, amependelea kuwatumia Alvaro Morata, Olivier Giroud na Tammy Abraham katika safu ya ushambuliaji.

Batshuayi alijiunga na Chelsea mwaka 2016 akitokea Marseille ya Ufaransa kwa Pauni 33 milioni lakini alishindwa kabisa kufanya kile kilichotarajiwa na kumfanya Kocha Antonio Conte, kumtegemea Diego Costa pekee katika ushambuliaji n ahata alipokuwa nje alimpanga Eden Hazard kuongoza mashambulizi.

Katika msimu wake wa kwanza alianza mechi 19 kati ya mechi 20 mchezo mmoja tu akitokea benchi na alifunga mabao matano.

Kuondoka kwa Costa aliyerejea Atletico Madrid ilikuwa nafasi nzuri kwa Batshuayi, kujihakikishia nafasi katika kikosi cha Chelsea lakini katika mechi 12 alizocheza hakufunga hata bao moja wala kusababisha jambo lililomkera Kocha Conte na kuamua kumuuza kwa mkopo.