Hernandez: Kashindwa Messi, Hazard nani bana!

BEKI wa Ufaransa, Lucas Hernandez amesema kwamba hawezi kuogoza kumkabili Eden Hazard kama aliweza kumdhibiti Lionel Messi kwenye fainali za Kombe la Dunia 2018 zinazoendelea huko Russia kwa sasa.

Hernandez kikosi chake cha Ufaransa kimetinga hatua ya nusu fainali ambapo kitakwaanza na Ubelgiji ya Hazard katika mechi hiyo. Hazard alicheza mpira mkubwa sana wakati Ubelgiji ilipoichapa Brazil 2-1 na kutinga hatua hiyo ya nusu fainali ambapo keshokutwa Jumanne watavaana na Les Bleus.

Ufaransa yenyewe imetinga nusu fainali baada ya kuichapa Uruguay 2-0, lakini waliwatoa pia Argentina kwa mabao 4-3 katika raundi ya 16 bora ya fainali hizo za Kombe la Dunia. Hernandez kwa sababu alimdhibiti Messi basi anaamini Hazard hawezi kusumbua.

“Hazard? Kumbukeni tumeshamtoa nje ya michuano mchezaji bora wa dunia, Messi,” alisema beki huyo anayechezea klabu ya Atletico Madrid, ambaye amekuwa akianzishwa kwenye mechi za Ufaransa katika fainali hizo.

“Hakugusa mpira. Tunaamini tutalifanya hilo tena tutakapokabiliana na Hazard.”