KPL yazikomalia Gor Mahia, Tusker kwa utovu wa nidhamu

Muktasari:

Wote wanatakiwa kufika mbele ya kamati huru ya kusimamia nidhamu na malalamiko (IDCC) siku za Jumatatu na Ijumaa ijayo.

Bodi ya Ligi Kuu ya KPL imezishitaki timu za Gor Mahia, Tusker FC na Muhoroni Youth pamoja na straika Stephen Waruru kwa kutokana na utovu wa nidhamu.

Wote wanatakiwa kufika mbele ya kamati huru ya kusimamia nidhamu na malalamiko (IDCC) siku za Jumatatu na Ijumaa ijayo.

Gor wameshtakiwa kwa kurusha chupa na mawe uwanjani wakati wa mechi yao dhidi ya Ulinzi wikiendi iliyopita mjini Kisumu.

Mashabiki wa Kogalo walisitisha mechi hiyo kwa zaidi ya dakika kumi baada ya Stephen Waruru kufunga bao la kuzawazisha dakika kumi kabla ya mechi kutamatika.

Mchezaji Waruru pia ameshtakiwa kwa kushangilia bao hilo mbele ya mashabiki wa Gor Mahia kwa njia isiyostahili.

Tusker kwa upande wao wameshtakiwa kukosa kutokubeba kadi za wachezaji wakati wa mechi yao ya ligi dhidi ya Zoo Kericho mjini Kericho Mei 10.