Gor Mahia yashinda kocha afura

Muktasari:

  • Matokeo hayo yamewafanya mabingwa wa Kenya kumaliza nafasi ya tatu ya mashindano Kombe la Kagame huku JKU wakiondoka wakiwa wa nne.

Dar es Salaam. Kocha wa Gor Mahia, Dylan Kerr amesema safu yake ya ushambuliaji haikuwa makini kutokana na kutengeneza nafasi nyingi na kushindwa kuzitumia katika ushindi wao wa mabao 2-0 dhidi ya JKU.
Matokeo hayo yamewafanya mabingwa wa Kenya kumaliza nafasi ya tatu ya mashindano Kombe la Kagame huku JKU wakiondoka wakiwa wa nne.
Bao la kuongoza la Gor Mahia lilifungwa dakika ya 52 na Francis Mustafa kabla ya dakika ya 89, Samuel Onyango kupachika bao la pili baada ya kupokea pasi safi ndani ya boksi kutoka kwa Jacques Tuyisenge.
Akizungumza mara baada ya mchezo huo alisema timu yake leo ilikuwa iibuke na ushindi wa zaidi ya mabao tisa kutokana na nafasi nyingi walizotengeneza, lakini wameshindwa kufanyaivyo kutokana na kukosa umakini.
"Timu yangu imecheza vizuri naipongeza, lakini kwa upande wa safu ya ushambuliaji imekosa umakini kwasababu wametengeneza nafasi zaidi ya tisa lakini wameshindwa kuzitumia," alisema Kerr.
Wakati huo huo kocha wa JKU, Hassan Ramadhan alisema bahati haikuwa upande wao wachezaji wake wameshindwa kuonyesha mchezo mzuri kama walivyofanya katika hatua ya robo fainali dhidi ya Simba.