Wema kama Malkia Chadema

Muktasari:

Wema Sepetu, anahudumiwa kama Malkia na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), baada ya kutangaza kukihama Chama Cha Mapinduzi (CCM).

BINTI mrembo mwenye wafuasi wengi kwenye mitandao ya kijamii,

Wema Sepetu, anahudumiwa kama Malkia na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), baada ya kutangaza kukihama Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Wema, tofauti na wanachama wengine wa Chadema waliojiunga katika miezi ya hivi karibuni, amepewa mlinzi maalumu ambaye atakuwa

akimlinda kwa kila atakapokuwa kutokana na kile Chadema wanachoeleza kwamba msanii huyo ni mtu muhimu.

Hali hiyo ilijidhihirisha juzi Ijumaa wakati alipowasili nyumbani kwao Sinza Kijitonyama kutoka kwenye mkutano wake na waandishi wa habari alikotangaza rasmi kuondoka CCM ingawa bado hajakabidhiwa kadi ya uanachama ya Chadema.

Aliwasili akiwa kwenye gari la kifahari, Toyota Land Cruizer V8 lenye namba za usajili T 830 DEW lenye rangi nyeusi na kufunguliwa mlango na mlinzi huyo.

Mlinzi huyo alikuwa makini muda wote akimfuata Wema kila mahali hadi alipokaa kwenye eneo lililoandaliwa maalum kwa mkutano huu, alisimama nyuma yake wakati Wema akizungumza na waandishi.

Awali mlinzi huyo aliwahi kuonekana kumlinda Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake Chadema(Bawacha) Halima Mdee ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kawe ambaye sasa imeelezwa kwamba yupo masomoni nje ya nchi.

Katibu wa Chadema Mkoa wa Dar es Salaam, Henry Kileo, aliliambia

Mwanaspoti akisema: “Kuna hofu kubwa kujitoa CCM, hivyo tunawapa

ulinzi ili kuwaondolea hofu hiyo na kuhakikisha usalama wao, sasa kama Wema ana nafasi yake kwa vijana, ni mtu maarufu.

“Tuna walinzi wengi, hivyo yeye kupewa huyo aliyekuwa anamlinda

Mdee. Si jambo la ajabu, ni mipango yetu makini kwenye ulinzi.”

Kujiunga Chadema

Wema alitangaza hatua hiyo sambamba na mama yake, Mariamu Sepetu, wakieleza kuwa wanahamia Chadema kusaka demokrasia.

Wema alisema mambo yaliyompata ameshangaa hakuna viongozi wa CCM waliojitokeza kuwa karibu naye, lakini pia wasanii wenzake walitishiwa hivyo kumtenga, hali ambayo imemfanya ajisikie mnyonge licha ya juhudi za kukitumikia chama hicho alizofanya hasa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu uliopita.

“Niliahidi ningefia CCM, lakini natamani ningejua mapema ndiyo

hivyo ya Mungu nimengi,nimetuhumiwa kilichofanyika kwangu ni uonevu, kweli tenda wema nenda zako usingoje shukrani,” alisema Wema.

“Dola ibaki ifanye kazi yake kama dola, wala sipo hapa kuikataza lakini iangalie haki za binadamu, isichukuliwe kwamba nimefanya uamuzi huu kwa hasira bali uamuzi wangu ni sahihi, nimeingia kwenye vita, nimevaa magwanda nipo tayari kupigana, nina imani kwamba kuna watu wapo nyuma yangu watanifuata,” alisema ambaye hivi karibuni aliingia matatani akihusishwa na biashara ya dawa za kulevywa. Shauri lake lipo kwenye vyombo vya sheria.