Walishtuka kijanja mapema

DULLY SYKES

Muktasari:

  • Mwanaspoti inakuletea orodha ya waimbaji wa muziki wa kizazi kipya nchini ambao waliona fursa mapema na kuamua kufungua studio na sasa wanakula maisha kilaini

KUNA baadhi ya wasanii wajanja sana. Licha ya kufanya vema kwenye fani huwa wanajisongesha kimtindo kwa kutambua kuwa wakati ukuta.

Uzoefu wanaokuwa nao kwenye fani, huwapa nafasi ya kuchangamkia fursa ya kuwa watayarishaji wa muziki, hivyo kujikuta hata kama kazi yake ya uimbaji itabuma, hawezi kupata stress kwa vile hupiga hela ndefu kama kawaida.

Mwanaspoti inakuletea orodha ya waimbaji wa muziki wa kizazi kipya nchini ambao waliona fursa mapema na kuamua kufungua studio na sasa wanakula maisha kilaini, hata kama shoo zimewakataa kutokana na ushindani uliopo ama umri kusogea.

Prince Dully Sykes

Msanii huyu mkongwe aliyetamba na nyimbo zake kali kinoma kwa wakati huo na mara nyingi kazi zake alikuwa akizitengeneza kwa Prodyuza Mika Mwamba, aliyekuwa akichuana miaka hiyo na wakali kama P. Funk na Master Jay wa MJ Records.

Dully baada ya kujishtukia kuwa umri unampa kisogo na asipokuwa makini atakuja kuchekwa, fasta alifungua studio inayofanya vema kwa sasa nchini.

Mkali huyo anamiliki studio hiyo ya 4.12 ambayo imefanya kazi nzuri sana kama Run Dsm ya P the Mc ambayo ndani yake kuna msanii Young Killer na Dully mwenyewe, lakini vile vile hata Na mimi nayo imefanywa katika studio hizo. Kitu cha kufurahisha ni kwamba, nyimbo zote za sasa za Dully amekuwa akijitengenezea mwenyewe hivi sasa hiki ni kipaji ambacho inawezekana amekipata kutokana na kutembea kwa watayarishaji wengi wakubwa.

Sir Juma Nature

Mkali huyu mwingine maarufu kama Kibla ni kati ya wasanii wachache ambao walikuwa wanakubalika kwa mtayarishaji mtata P Funk Majani. Sir Nature ngoma zake zote za zamani zilikuwa zina mdundo mzito kutoka studio za Bongo Record kama ile ngoma ya Ugali, Sitaki Demu na Hakuna Kulala.

Lakini, baada ya kupishana kauli na kuunda kundi lake la Wanaume Halisi aliamua pia kufungua studio ya Halisi Records ambayo alifanya ngoma zake kadhaa.  Licha ya kumiliki studio, lakini bado aliendelea kurudi kwa Majani kwani mjanja wake na kutoa ngoma kama ‘Dogo’ ambayo ilibamba kinoma.

Quick Rocka

Quick ni kichwa kutoka katika kundi la Rockers Family, jamaa katamba na ngoma zake kadhaa, lakini baadaye akausoma upepo na kuona kuwa kama atachelewa sana akitegemea kuimba peke yake itakula kwake, hivyo akaanzisha studio zake.

Awali, mwenyewe alikuwa akitaka kuifanya kama Home Studio, lakini baadhi ya washikaji zake ambao ni watayarishaji walimshauri kuifungua na mpaka hivi sasa studio hiyo imefanya kazi nyingi kali pamoja na kazi mpya ya Joh Makini inayokwenda kwa jina la Waya inayobamba mtaani.

NahreEl

Huyu ni mkali kwa midundo ya Hip Hop, wasanii kutoka kundi la Weusi wote walikuwa wanafanyia kazi zao hapa, lakini baadaye wakaamia kwa Rufa. Hata hivyo, Nahreel anastaili sifa zake juu ya uatayarishaji wake hatari.

Nahreel bado anaendelea kutengeneza kazi zake huku akiimba na mpenzi wake na kuunda kundi la NavyKenzo, ambalo lina nyimbo kali kama Kamatia Chini na nyimbo nyingine kali.

Mesen Selekta

Hivi sasa amegeukia nyimbo za singeli akiwa na msanii wake Sholo Mwamba. Jamaa anaimba, huku pia anagonga biti nzito za kuchezeka na ukisikia tu Defatality Music basi ujue humo kuna mikono ya Mesen Selekta.

Mesen pia hana roho ya kubana kwa sababu alimchukua mdada Pam D na wakafanya ngoma ambazo zilimtambulisha mdada huyu na mpaka leo hii wanaendelea kuwa pamoja hii ni hongera kwao wote kwasababu kukaa pamoja kwa muda mrefu kama kaka na dada bila kuzinguana kimahusiano ya mapenzi katika kazi nayo ni kazi pia.

Man Water

Man Maji wala usibishe? Najua utabisha lakini ukweli ndio huo huyu jamaa naye ni msanii. Labda nikukumbushe kidogo, katika nyimbo ya Mr Blue ya Love Me the Way Iam, huyu jamaa sauti yake imehusika mule sasa na ndiye katengeneza wimbo ule.

Katika nyimbo ya Dushelele ya Ali Kiba nayo ameweka sauti yake vile vile na hivi sasa yupo katika kituo kimoja cha habari amewekwa katika kutengeneza matangazo na hii ni kutokana na sauti yake jinsi ilivyo.

Ila anakumbukwa zaidi kwa ufanisi wake wa kumpa jina kubwa Twenty Percent (20%) hadi kutambulika ndani na nje ya Bongo.