Pacha wa Klopp aduwaza wengi kikosini Liverpool

Muktasari:

Lucas aliitwa na kocha Jurgen Klopp kupewa maelekezo wakati Liverpool ilipomenyana na Tottenham Hotspur kwenye Kombe la Ligi, lakini kwenye benchi hilo alisimama kocha msaidizi, ambaye anafanana kweli kweli na Klopp.

KIUNGO wa Liverpool, Mbrazili Lucas Leiva alibaki kwenye mshangao kwa dakika kadhaa kitu ambacho kiliwashangaza pia mashabiki wa timu hiyo waliofurika uwanja wa Anfield, walipoona watu wawili wanaofanana kweli kweli kwenye benchi la timu hiyo.

Lucas aliitwa na kocha Jurgen Klopp kupewa maelekezo wakati Liverpool ilipomenyana na Tottenham Hotspur kwenye Kombe la Ligi, lakini kwenye benchi hilo alisimama kocha msaidizi, ambaye anafanana kweli kweli na Klopp.

Kitu hicho kiliwaduwaza pia mashabiki wa Liverpool. Kocha wa viungo, Andreas Kornmayer, anafanana sana na Klopp na jambo hilo limekuwa likiwapa shida wachezaji na mashabiki wakishindwa kuwatambua kutokana na kuonakana kama pacha.

Kornmayer alijiunga na Liverpool akitokea Bayern Munich kwenye dirisha lililopita la usajili na ndiye mtu anayehusika na soka la kasi linalochezwa na miamba hiyo ya Anfield kwa sasa. Kornmayer ni shabiki pia wa Klopp na ndiyo maana anajaribu kujifananisha na kocha huyo katika mazingira yote.