Zidane kutua Man Utd na nyota wanne

Muktasari:

  • Zidane aliiongoza Real Madrid kupata ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya mara tatu kabla ya kuondoka Bernabeu mwishoni mwa msimu uliopita.

KOCHA wa zamani wa Real Madrid, Zinedine Zidane ni kama anasubiri kipyenga tu cha kocha Jose Mourinho kutimuliwa Manchester United ili atue.

Hiyo imethibitika baada ya kocha huyo kutengeneza orodha ya wachezaji atakaowataka  katika kikosi chake iwapo atatua Manchester United.

Zidane aliiongoza Real Madrid kupata ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya mara tatu kabla ya kuondoka Bernabeu mwishoni mwa msimu uliopita.

Kocha wa Manchester United Jose Mourinho anafahamu hilo na ndio maana alitumia presha hiyo kuhakikisha wanashinda mechi dhidi ya Burnley wiki iliyopita.

Kuwepo kwa Mourinho katika kikosi hicho, inategemea ushindi wake katika siku za karibuni, na kama akishindwa kufanya hivyo, panga litamuhusu.

Zidane, ambaye wiki hii aliweka wazi kwamba hatosita kujiunga na Manchester United iwapo ataitwa, ameshaanza kujipanga kuhakikisha anaweka mambo sawa kabla ya kuanza kazi.

Imefahamika, Zidane anaona ana uwezo wa kuonyesha kiwango cha maana hapo Ligi Kuu ya England na hayo yanaweza kutokea iwapo uongozi wa klabu hiyo ukiwanunua Toni Kroos, James Rodriguez, Thiago na  Edinson Cavani.