Zari amruka Diamond, ataka asimchezee

Muktasari:

Amemtaka Diamond asimchezee hata kama yeye ni mama wa watoto wake

Dar es Salaam. Drama za sakata la Diamond na mwanamitindo Hamisa Mobetto limechukua sura mpya baada ya Zari kujibu mapigo katika mtandao wa Snapchat akionya asihusishwe.
Awali katika maelezo yake mwanamuziki Diamond amesema ameshazungumza na mpenzi wake huyo kuhusiana na mtoto aliyezaa na Hamisa na kwamba ameelewa na hakuna tatizo tena.
Wakati Diamond akiendelea na mahojiano katika kituo cha Clouds FM, Zari aliandika katika mtandao huo akisema: “Hahahaha unajidanganya, unasema uongo kuhusu mimi kujua kuhusu michepuko yako, malizana na balaa ulilolianzisha. Mimi kunyamaza haimaanishi ni mpumbavu. Kuwa makini na maneno yako.”
 Aliendelea kuandika: “Inawezekana mimi ni mama wa watoto wako ndio maana nimeamua kunyamaza kimya. Labda ugoogle kuhusu ‘defamation of character law suit’, usinijaribu.”
Diamond alipoulizwa kuhusu kauli hizo amesema anamwelewa kwa kuwa kuna baadhi ya mambo hakumweleza na kwa mara ya kwanza huenda ameyasikia wakati huo.