Yule mkalimani 'mtata' wa Mwakinyo aibua mengine

Muktasari:

  • Chid ambaye aliongozana na Mwakinyo kwenda England kwa ajili ya kuzichapa na Sam Eggington ambaye alimpiga katika raundi ya pili akaokolewa na mwamuzi ( Technical  Knock Out)

Dar es Salaam. Yule mkalimani, Rashid Nasoro 'Chid' aliyeibua mapya baada ya pambano la bondia, Hassan Mwakinyo kumalizika, amewafichua wazito kwenye viti vyao, wakatoa neno.
Chid ambaye aliongozana na Mwakinyo kwenda England kwa ajili ya kuzichapa na Sam Eggington ambaye alimpiga katika raundi ya pili akaokolewa na mwamuzi ( Technical  Knock Out)
Alijikuta maarufu kutokana na kituko alichokifanya baada ya kutafsiri maneno ya Kiswahili kwenda Kiingereza kwenye vyombo vya habari tofauti na yaliyozungumzwa.
Na kutokana na hali hiyo, kamati ya kusimamia mamlaka ya ngumi za kulipwa Tanzania,  imeweka utaratibu wa kuwataftia mabondia wakalimani maalumu na watatoka humo kila watakapokuwa wanakwenda nje ya nchi kwenye mapambano.
"Utaratibu huu haukuwepo, lakini utaanza hivi karibuni ambapo bondia atakayekwenda kuzichapa nje ya nchi katika msafara wake, atakuwepo mkalimani kutoka kwenye kamati," alisema Makamu Mwenyekiti wa Kamati, Jovic Aness.
Amesema, kitendo cha Chid kuzungumza tofauti na alichokisema Mwakinyo hakikuwa sahihi kwani angeeleza yale ambayo bondia aliyazungumza ndipo aongeze mengine aliyohitaji.