Yanga yashusha nyota wake wapya

Muktasari:

  • Mazoezi hayo yalifanyika jana asubuhi kwenye Uwanja wa Uhuru, jijini Dar es Salaam chini ya Kocha George Lwandamina na wasaidizi wake, ambapo asilimia kubwa ya wachezaji waliosajili na timu hiyo na wale wa zamani walishiriki.

Dar es Salaam.Mabingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga imeanza mazoezi ya uwanjani, ikiwa na nyota wake wapya wakiwamo Mkameruni, Fernando Bongyang na Mnigeria Henry Tony Okoh walipiga mpira mwingi, huku Kiberenge Burhan, Yahya Akilimali akifunika zaidi.

Mazoezi hayo yalifanyika jana asubuhi kwenye Uwanja wa Uhuru, jijini Dar es Salaam chini ya Kocha George Lwandamina na wasaidizi wake, ambapo asilimia kubwa ya wachezaji waliosajili na timu hiyo na wale wa zamani walishiriki.

Kipa Youthe Rostand, Ibrahim Ajib, Akilimali na nyota hao wa kigeni wanaowania nafasi moja iliyosalia walionyesha uwezo wao, japo kiungo rasta kutoka Swaziland, Tshishimbi Kabamba 'Papii' hakuwepo kabisa uwanjani hapo.

Kocha Lwandamina alisema ameanza vizuri kuwaona vijana wake na anaimani ataendelea kuwasoma kadri wakiendelea kujifua baada ya kutumia wiki mbili na ushei kwenye mazoezi ya Gym.