Wakenya waiteka Ngorongoro Marathoni

Muktasari:

Tanzania washindwa kufurukuta mbio za Ngorongoro

Karatu. Wanariadha wa Kenya wameendelea kutamba katika ardhi ya Tanzania baada ya kunyakuwa medali ya dhahabu kwa wanawake na wanaume katika mashindano ya Ngorongoro marathoni.

Mwanariadha wa Kenya, Joseph Mbatha alimaliza wa kwanza katika mbio hizo za umbali za km 21 akitumia saa 1:04:54 na kujinyakulia Sh 1milioni na medali.

Nafasi ya pili ilikwenda kwa Mkenya Berdarn Mussa aliyetumia saa 1:05:09 na kushindia medali na kitita cha shilingi laki tano na Mtanzania Pascal Mombo akiambulia nafasi ya tatu na kupewa shilingi laki mbili na nusu baada ya kumaliza km 21 kwa kutumia saa 1:06:05.

Kenya iliendeleza ubabe katika mbio hizo za Ngorongoro baada ya Monica Cherito kuchukua ubingwa kwa wanawake baada ya kumaliza km 21, akitumia 1:04:54 na kupewa zawadi ya medali na shilingi milioni moja akifuatiwa na Failuna Abdi wa Tanzania aliyemaliza kwa muda wa saa 1:06:12 alizawadiwa medali na shilingi laki tano.

Mshindi watatu imeenda kwa Tanzania kupitia Fadhila Salum aliyepa zawadi ya medali na shilingi laki mbili nusu.

Katika mbio za kilomita tano wanaume Elibariki Buko wa JKT alifanikiwa kutwaa ubingwa akimaliza kwa dakika 14:14:81 akifuatiwa na Marco Sylvester Wa JKT kwa dakika 14:14:86 huku Sylvester Simon wa Polisi akimaliza nafasi ya tatu kwa kutumia dakika 14:22:83.

Kwa wanawake Merry Naali kutoka AAAC alitwaa ubingwa baada ya kumaliza  kwa kutumia dakika 17:40:65 akifuatiwa na Rozali Fabiano wa JKTkt aliyetumia dakika 17:55:26 huku nafasi ya tatu ikichukuliwa na Anastazia Mkama wa Mara akimaliza kwa kutumia dakika 18:01:40

Mbio za  watoto walioshindana km 2.5 wanaume Damian Christian , Simon Michael na Ramadhan miraji walipata zawadi. Kwa wasichana km 2.5 Neema Victor, Christina faustine na Lucia Mochema walipata zawadi.