Vita ya kushuka daraja sio mchezo asee

Muktasari:

  • Ratiba za kila mmoja katika michezo yao iliyobaki, ndiyo itakayowabeba na kuonyesha kama wanaweza kusalia ama kushuka na nafasi zao kuchukuliwa na vilabu ambavyo vimepanda.

Majimaji, Ndanda na Njombe Mji ndio timu ambazo zipo katika wakati mgumu hivi sasa baada ya kushika nafasi tatu za chini huku kila mmoja akiwa amebakiza mchezo mmoja huku  wakihitaji ushindi ili kujihakikishia nafasi ya kubaki katika ligi.

Ratiba za kila mmoja katika michezo yao iliyobaki, ndiyo itakayowabeba na kuonyesha kama wanaweza kusalia ama kushuka na nafasi zao kuchukuliwa na vilabu ambavyo vimepanda.

Majimaji wametoka kupoteza dhidi ya Azam baada ya kupokea kichapo cha 2-0, wakaenda kupoteza dhidi ya Singida United 3-2 lakini wamebakiza mchezo na Simba, mechi ambayo kiuhalisia itakuwa ngumu kwa upande wao.

Majimaji licha ya kwamba watakuwa wenyeji katika mchezo dhidi ya Simba, bado watakuwa katika wakati mgumu katika mechi hiyo, kwani Simba inawezekana wasikubali kuendelea kuchafuliwa kwa kufungwa mechi mbili mfululizo, baada ya kupokea kichapo cha 1-0 kutoka kwa Kagera Sugar na kuvunjiwa rekodi yao ya kutopoteza msimu huu.

Njombe Mji ambao ndio wanashika mkia wakiwa na pointi 22, walipoteza dhidi ya Kagera Sugar, wamejikuta wakiwa katika hali ngumu tena baada ya kupokea kichapo cha 1-0 kutoka kwa Mtibwa Sugar.

Timu hiyo imebakiza mchezo mmoja dhidi ya Mwadui, lakini Mwadui ambao nao watacheza katika uwanja wao wa nyumbani, bado watakuwa katika wakati mgumu kwani Mwadui inayoshika nafasi 10 ikiwa na pointi33,  haitokubali kupoteza mchezo huo kwasababu kocha Ally Bizimungu anataka kuweka rekodi yake ndani ya kikosi hicho.

Kwa upande wa Ndanda ambao wanashika nafasi ya 15 wakiwa na pointi 23 katika michezo 28 waliyocheza, wao wanaweza kusalia kutokana na ratiba yao kutokuwa ngumu sana.

Ndanda  wamebakiza michezo miwili dhidi ya Mwadui na Stand United ambayo yote watacheza katika uwanja wa Nangwanda Sijaona, huku Stand United inayoshika nafasi ya 9 ikiwa na pointi 32 katika michezo 27 waliyocheza, hawana cha kupoteza msimu huu kutokana na kuwa salama, lakini Ndanda watajikuta katika wakati mgumu dhidi ya Mwadui kwasababu haipo tayari kupoteza lakini pia ushindi walioupata dhidi ya Yanga ni kama umeongeza morali katika kikosi hicho.