Timu ya Taifa wanawake Kenya yajiweka patamu Cosafa

Muktasari:

  • Starlets watachuana na Zambia alasiri hii baada ya kupigwa 4-0 na Zimbabwe mechi ya nusu fainali juzi Alhamisi.

Timu ya taifa ya wanadada, Harambee Starlets watawania nafasi ya tatu kwenye mashindano ya Baraza la Vyama vya Soka kanda ya Afrika Kusini (COSAFA) yanayoendelea nchini Zimbabwe.

 

Starlets watachuana na Zambia alasiri hii baada ya kupigwa 4-0 na Zimbabwe mechi ya nusu fainali juzi Alhamisi.

 

Kocha Richard Kanyi alikiri vipusa wake walilemewa kisaikolojia na wenyeji na kufanya makosa yaliyoikosti timu.

 

“Hatukujiandaa kiakili kupambana nao tukaishia kufanya makosa hapa na pale yaliyochangia kichapo. Walikua na faida ya kuwa nyumbani. Hata hivyo, tumejitahidi manake tulikuja huku kama wageni kufika nusu fainali ni mafanikio ya aina yake. Tutapambana tuone kama tunaweza kumaliza nafasi ya tatu leo,” alisema Kanyi.

 

Kocha wa Zimbabwe Sithethelelwe Sibanda aliwasifia Starlets kwa mchezo wa kufana katika mashindano hayo, “Kenya ina timu nzuri imekuja huku ikaonyesha kwamba wana kikosi cha kupigiwa mfano. Kwa kweli wana kesho ya kufana wakibakiza kikosi hichi.”

 

Kenya ilimaliza kileleni mwa kundi B kufuatia matokeo mazuri dhidi ya Mozambique, Mauritius na Swaziland mechi walizoshinda 5-2, 11-0 na 1-0 mtawalia