Tenga asaka ubosi Fifa

Muktasari:

  • Nafasi hiyo ni ile iliyoachwa wazi na Rais wa Shirikisho la Soka la Ghana (GFA), Kwesi Nyantakyi aliyefungiwa na FIFA.

Dar es Salaam. Rais wa zamani wa TFF na Mwenyekiti wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Leodegar Tenga amepitishwa na kamati ya maadili ya Shirikisho la Soka Duniani (FIFA), kuwania nafasi ya mjumbe wa Baraza la Shirikisho hilo akiwakilisha kundi la nchi za Afrika zinazozungumza lugha ya Kiingereza.

Nafasi hiyo ni ile iliyoachwa wazi na Rais wa Shirikisho la Soka la Ghana (GFA), Kwesi Nyantakyi aliyefungiwa na FIFA.

Jumla ya viongozi watano wa mpira wa miguu kutoka nchi mbalimbali barani Afrika wamepitishwa kuwania nafasi hiyo sambamba na Tenga.

Ukimuondoa Tenga ambaye pia ni Mjumbe wa kamati ya utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF), wagombea wengine ni Danny Jordaan (Afrika Kusini), Nick Mwenda (Kenya), Elvis Chetty (Shelisheli) na Walter Nyamilandu (Malawi).

Katika mchujo huo uliompitisha Tenga, Rais wa Shirikisho la Soka Uganda (FUFA), Moses Magogo na Adam Methethwa wa Swaziland walienguliwa kuwania nafasi hiyo.

Uchaguzi wa kumpata mshindi wa nafasi hiyo linatarajiwa kufanyika jijini Cairo, Septemba 28.