Simba yaifunika Yanga kimataifa

Muktasari:

Simba pia ameshika nafasi 602 katika klabu bora duniani wakati Yanga imeshindwa kutajwa katika orodha hiyo ya timu 1000 bora za miaka 10 ya mwanzo wa karne 21 wakiongoza Barcelona, wakifuatiwa na Manchester United na Liverpool.

Dar es Salaam. Simba imeendelea kuigalagaza Yanga katika viwango vya ubora wa kimataifa akiwa nafasi 63, huku watani zao wa jadi wapo nafasi 157, kati ya klabu 274 bora barani Afrika katika muongo wa kwanza (2001-2010) wa karne ya 21.

Kwa mujibu wa ripoti iliyochapishwa Machi 26,2018 katika tovuti ya http://www.iffhs.de inayojihusisha na utoaji wa takwimu za michezo duniani umeonyesha katika miaka 10 ya mwanzo ya Karne ya 21, Simba imeongoza kwa ubora ikiwa ya 63 na pointi 383.5, wakati mabingwa wa Ligi Kuu Yanga wakiwa nafasi ya 157 na pointi 222.5 wakati Mtibwa Sugar ipo nafasi 165 na pointi 218.

Simba pia ameshika nafasi 602 katika klabu bora duniani wakati Yanga imeshindwa kutajwa katika orodha hiyo ya timu 1000 bora za miaka 10 ya mwanzo wa karne 21 wakiongoza Barcelona, wakifuatiwa na Manchester United na Liverpool.

Kwa Afrika, Al-Ahly Cairo imeendelea kung’ara ikiwa ndiyo klabu bora zaidi katika muongo wa kwanza wa karne ya 21.

Katika orodha hiyo klabu mbili za Misri na mbili za Tunisia zimeingia katika 10 bora kati ya hizo tatu zinaongoza katika orodha hiyo.

Klabu bora ya Afrika kwa karne 20, Asante Kotoko Kumase (Ghana) yenye sasa imeangukia nafasi ya 11.

Katika orodha ya timu 100 bora, zinatoka katika mataifa 21. Nchi zilizokuwa na klabu nyingi katika orodha hiyo “Top 100″ ni: Algeria (11), Nigeria (11), Afrika Kusini (9), Misri (8), Morocco (8), Zambia (8), Cameroon (7), Tunisia (6), Ghana (6), Angola (5) na Ivory Coast (4).

Katika kipindi cha kuanzia 2001-2010, klabu 268 za Afrika ziliambulia kupata zaidi ya pointi 150.