Shearer amponda Rashford hadharani

Muktasari:

  • Rashford mshambuliaji wa Manchester United alimwagiwa sifa alipomfunga kirahisi mchezaji mwenzake wa United, anayeidakia Hispania, David de Gea alipounganisha pasi ya Luke Shaw, katika mashindano ya Uefa Nations League.

London, England. Licha ya Marcus Rashford kuifungia England bao katika kichapo cha mabao 2- 1 kutoka kwa Hispania, nguli wa Newcastle United, Allan Shearer amemponda kinda huyo.

Rashford mshambuliaji wa Manchester United alimwagiwa sifa alipomfunga kirahisi mchezaji mwenzake wa United, anayeidakia Hispania, David de Gea alipounganisha pasi ya Luke Shaw, katika mashindano ya Uefa Nations League.

Wakati baadhi ya watu wakimpongeza chipukizi huyo, mshambuliaji mahiri wa zamani wa England, Shearer, alipinga akisema Rashford ndiye aliyeinyima nchi yake ushindi katika mchezo huo uliopigwa kwenye Uwanja wa Wembley.

Alisema kwa namna alivyoushuhudia mchezo huo, Rashford alikosa mabao kadhaa ambayo yangeiwezesha nchi yake kuibuka na ushindi katika mchezo huo.

“Sidhani kama Rashford anastahili kuendelea kuichezea timu ya Taifa kwa kiwango hiki, alipata nafasi nyingi za kufunga mabao, lakini hakufanya hivyo bila shaka kufungwa huku kumetokana na yeye kupoteza nafasi nyingi,” alisema Shearer.

Shearer alikiri kuwa na shabiki wa Rashford mwenye miaka 20 lakini akasema wazi kuwa kama hatabadilika hastahili kuendelea kupewa nafasi ya kulitumikia Taifa.

Alisema kwa nafasi nzuri alizozipata mchezaji huyo katika kipindi cha kwanza pekee alipaswa kuondoka uwanjani akiwa amefunga mabao matatu ‘hat trick’ lakini yeye aliridhika kuondoka na bao moja.

Shearer aliendeela kusema kuwa sasa amefahamu kwamba Kocha wa Manchester United, Jose Mourinho yupo sahihi kutomuanzisha mchezaji huyo kuongoza mashambulizi kwa kuwa hayupo makini katika kufunga.