Sanchez kama Di Maria Man Unitedmwanaspoti,michezo

Muktasari:

Sanchez ameanza kufananishwa na kiungo wa pembeni wa zamani wa timu hiyo Angel Di Maria.

London, England. Maisha ya mshambuliaji wa Manchester United, Alexis Sanchez yametajwa kuwa magumu zaidi tofauti na matarajio yake.

Sanchez ameanza kufananishwa na kiungo wa pembeni wa zamani wa timu hiyo Angel Di Maria.

Mchezaji huyo wa kimataifa wa Argentina alitua Man United kwa mbwembwe kutoka Real Madrid akiwa kwenye kiwango bora, lakini aliishia kusota benchi.

Di Maria alitimka Old Trafford na kujiunga na Paris Saint Germain (PSG) ili kulinda kiwango chake ambapo amekuwa tishio katika Ligi Kuu Ufaransa.

Sanchez, nyota wa kimataifa wa Chile anapitia kipindi kigumu Man United, baada ya kutua kwa mbinde mikononi mwa kocha Jose Mourinho kutoka Arsenal.

Hata hivyo, mshambuliaji ameshindwa kucheza kwa kiwango bora kama ilivyotarajiwa licha ya kulipwa mshahara mkubwa zaidi England Pauni 600, 000 kwa wiki.

Sanchez amefunga moja katika mechi 10 alizocheza Man United na tayari ameanza kupigiwa kelele na wadau wa mchezo wa soka duniani.

Mourinho alimuweka benchi kwa mara ya kwanza katika mchezo wa Kombe la FA walioshinda mabao 2-0 dhidi ya Brighton.

Man United imekiri Sanchez mwenye miaka 29, anapambana kurejesha makali na anapitia kipindi kigumu cha maisha yake ya soka.

Maofisa wa Man United wamebaini Sanchez  hana furaha na mara kadhaa ameonekana akiwa peke yake katika mgahawa wa klabu hiyo.