Samatta kununua ndege yake binafsi

Muktasari:

Samatta amesema, katika 'vurugu' zake zote za uwanjani suala la kumiliki ndege liko kwenye akili yake na mambo yakimwendea poa, atakamilisha.

Dar es Salaam. Huwezi kuamini lakini hiki unachokisoma hapa ndiyo ukweli mtupu kuwa mshambuliaji wa Genk ya Ubelgiji na nahodha wa Taifa Stars, Mbwana Samatta yuko mbioni kumiliki ndege yake  binafsi.

Samatta amesema, katika 'vurugu' zake zote za uwanjani suala la kumiliki ndege liko kwenye akili yake na mambo yakimwendea poa, atakamilisha.

Mshambuliaji huyo tegemeo ndani ya kikosi hicho kinachotikisa Ligi Kuu Ubelgiji, amesisitiza licha ya kuwa si kila ndoto inaweza kukamilika lakini atapambana hadi kieleweke.

Na ameandika maneno haya 'mazito' katika ukurasa wake wa Instagram: "Ndoto za kumiliki ndege binafsi (private jet)  zimeanza baada ya kupiga picha hii, si kila ndoto inaweza kutimia ila, acha vita ianze."

Katika ujumbe huo, kuna picha inayomwonyesha Samatta akiwa pembeni ya ndege nzuri ya kisasa yenye nembo ya klabu yao ya Genk na jamaa mwingine aliyevaa sare kama za jeshi.