Salim Mbonde kutimkia Afrika Kusini

Muktasari:

Mbonde alipata maumivu ya goti mwanzoni mwa msimu huu katika mchezo wao wa ligi kuu dhidi ya Mtibwa Sugar  mechi ilichezwa Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Dar es Salaam: Beki wa Simba na Taifa Stars, Salim Mbonde, ataondoka kwenda nchini Afrika Kusini muda wowote kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi na matibabu ya goti linalomsumbua.

Mbonde alipata maumivu ya goti mwanzoni mwa msimu huu katika mchezo wao wa ligi kuu dhidi ya Mtibwa Sugar  mechi ilichezwa Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Alifanyiwa matibabu akapata nafuu na baadaye akarudi uwanjani kucheza lakini baada ya mechi mbili tu, maumivu yakamrudia kwa mara nyingine katika mchezo wao wa ligi kuu dhidi ya Kagera Sugar alipoingia kuchukua nafasi ya Mghana James Kotei.

Katika mchezo huo ambao kwake, Wanasimba na taifa kwa ujumla ulikuwa wa kihistoria kwani ndiyo siku ambayo walikabidhiwa kombe la ubingwa wa Ligi Kuu Bara na Rais John Magufuli.

Alipoingia tu kipindi cha pili, hakucheza dakika nyingi akatolewa nje baada ya maumivu kumzidi jambo lililomfanya atoe chozi la uchungu.

Amesema, tukio hilo limemuumiza: "Inaniuma sana, nimerudi uwanjani nikijua sasa nitacheza lakini matokeo yake ndiyo kama hivyo nimeumia tena. Lakini kitu kikubwa ninachoshukuru ni kwamba,  mabosi wangu wamenihakikishia kuwa watanipeleka Afrika Kusini kwa ajili ya uchunmguzi zaidi."

Amesema, kama atakwenda Afrika Kusini hiyo ndiyo faraja kwake kwa sababu anaamini matibabu atakayoyapata huko yatakuwa ya kina na akifanikiwa kupona kabisa na kurudi uwanjani itakuwa uhakika.