Ronaldo aharibu sherehe ya Yanga, watoka sare 1-1

Muktasari:

  • Kwa matokeo hayo, Yanga inaendelea kushika nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi kuu ikiwa na pointi 48 na Simba akiendelea kutamba kileleni na pointi 59.

MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu Bara wameshindwa kutamba mbele ya Mbeya City baaya ya kulazimishwa kwa sare ya bao 1-1 kwenye Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.

Ni Idd Seleman 'Ronaldo' aliyeisawazishia Mbeya City dakika ya 90 ya mchezo akipokea pasi  kutoka upande wa kulia kwake na kufanya mchezo huo kumalizika wakiwa wamegawana pointi moja moja.

Yanga ambao wamefikisha pointi 48 baada ya mchezo huo, walipata bao lao mwanzoni mwa kipindi cha pili katika dakika 57 kupitia kwa Raphael Daud ambaye aliunganisha mpira wa adhabu iliyopigwa na Juma Abdul.

Mchezo huo uliokuwa na ushindani wa hali ya juu na ulisimama mara kwa mara kutokana na vurugu tofauti zilizotokea uwanjani hapo waliokuwa wakirusha mawe uwanjani.

Hata hivyo, dakika ya 65 beki wa Mbeya City,  Ramadhan Malima alionyeshwa kadi nyekundu na mwamuzi, Shomari Lawi. Adhabu hiyo ni kutokana na kadi mbili za njano baada ya kumchezea vibaya Yusuph Mhilu.

Kutokana na matokeo hayo, Yanga inaendelea kushika nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi kuu akiwa na pointi 48 na Simba ikiendelea kutamba kileleni na pointi 59.