Rais Magufuli sasa rasmi kuikabidhi Simba kombe

Dar es Salaam. Kaimu Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Wilfred Kidao amesema kwamba Rais John Magufuli amethibitisha mwaliko wa kwenda Uwanja wa Taifa kukabidhi kombe kwa klabu ya Simba itakapokutana na Kagera Sugar siku ya Jumamosi kwenye mchezo wa Ligi Kuu.

Kidao ametoa taarifa hiyo mbele ya waandishi wa habari leo Jumatano, ikiwa ni siku moja tangu Rais wa TFF, Walace Karia atangaze kumuomba mkuu huyo wa nchi kuikabidhi Simba kombe la ubingwa.

Katibu huyo mkuu alisema, Rais Magufuli amethibitisha kupitia Waziri wa Habari, Michezo, Sanaa na Utamaduni, Dk Harrison Mwakyembe kuwa atakuwa mgeni rasmi katika sherehe hizo za kuikabidhi Simba taji la ubingwa msimu huu.