Pesa zavuruga mastaa Ingwe

Muktasari:

Hata hivyo, kiulingana na ofisa mmoja wa Ingwe (Jina limebanwa), bado klabu haijapokea hela hizo kutoka kwa wadhamini Multi Choice na ndicho kitu wanachopaswa kuelewa wachezaji wao.

WACHEZAJI wa AFC Leopards wamewavimbishia vichwa wasimamizi wa klabu kuhusiana na zawadi ya Sh2 milioni ambazo hawajapokea ikiwa ni wiki ya tatu toka waliposhinda taji la Gotv Shield Cup.

Ingwe waliwalaza Kariobangi Sharks 2-0 Oktoba 23 kwenye fainali ya kombe hilo na kujishindia zawadi ya senti hizo pamoja na nafasi ya kuiwakilisha taifa kwenye dimba la CAF mwaka ujao.

Hata hivyo, mpaka wa leo wachezaji wanadai hawajapokea senti hizo na wamekuwa wakiiipa presha menejimenti wakitaka kujua ni kwa nini mpaka muda huu hela hizo hawajatiliwa kwenye akaunti zao.

 “Wachezaji wamekuwa wakitupa presha wiki nzima wakitaka hela hizo, lakini bado hatujapokea kutoka kwa wadhamini. Huu ndio ujumbe wanaopaswa kuelewa. Wadhamini walituambia tusubiri hadi baada ya marudio ya uchaguzi wa Rais na tumetulia mpaka sasa kwa sababu tunawaamini watatupa mwishowe,” afisa huyo amesema.