Okwi, Kagere waanza tizi Simba, Niyonzima na Juuko ndio kama vile!

Muktasari:

  • Okwi na Kagere walikuwa kwenye majukumu ya timu zao za Taifa, Kagere Rwanda 'Amavubi' na Okwi Uganda 'The Cranes', lakini baada ya kumaliza wamerejea na kuendelea na mazoezi hayo.

 Dar es Salaam. Wachezaji wa Simba, Emmanuel Okwi na Meddie Kagere wamerejea kwenye kikosi chao na jioni ya leo Jumatano, wameanza mazoezi ya pamoja na wenzao katika Uwanja wa Boko Veterani.

Okwi na Kagere walikuwa kwenye majukumu ya timu zao za Taifa, Kagere Rwanda 'Amavubi' na Okwi Uganda 'The Cranes', lakini baada ya kumaliza wamerejea na kuendelea na mazoezi hayo.

 Kagere na Okwi walifika mazoezini hapa wakiwa na morali ya hali ya juu na wakaanza kufanya mazoezi ya kupasha misuli kama changamsha bwege pamoja na wenzao kabla ya mazoezi rasmi.

 Licha ya Okwi na Kagere kuwasili, Juuko Murshid na Haruna Niyonzima ambao pia walikuwa kwenye timu zao za taifa, hawakuonekana. Juuko alikuwa na The Cranes wakati Niyonzima alikuwa na Amavubi.

Simba inajiandaa na mchezo dhidi ya Ndanda FC, utakaopigwa Jumamosi hii katika uwanja wa Nangwanda, Sijaona mkoani Mtwara.