Niyonzima amepania mjue!

Muktasari:

Niyonzima yuko nchini Kenya pamoja na kikosi chake cha Simba kwa ajili ya kushiriki mashindano ya SportPesa yanayoanza kutimua vumbi leo Jumapili.

Nakuru: Kiungo wa Simba, Haruna Niyonzima amesema ataitumia michuano ya SportPesa kuendelea kujiweka 'fiti' kwa ajili ya msimu ujao wa ligi kuu na mashindano.

Niyonzima aliyejiunga na Simba msimu uliopita akitokea kwa watani wao wa jadi Yanga,  alikosekana kwenye kikosi cha timu hiyo kwa muda mrefu kutokana na majeraha ya goti kabla ya kurejea kwenye mechi za mwisho.

Kiungo huyo Mnyarwanda amesema yeye pamoja na wachezaji wengine ambao walikuwa hawapati muda wa kucheza kwenye ligi msimu uliopita, hii ni fursa kubwa kwao kujiweka 'fiti' zaidi.

“Mchezaji kama hupati nafasi ya kucheza hata kiwango chako kinakuwa tatizo. Nafurahi kwamba nimerejea, nitatumia mechi hizi za SportPesa kuendelea kujiweka 'fiti' zaidi,” amesema.