Ngassa: Hawa Simba mbona wanapigika tu

Muktasari:

  • Ngassa ameliambia Mwanaspoti kwamba hakutaka kuzungumza awali kwani alitaka kujiridhisha na amebaini kuwa timu yao ina kikosi cha maana chenye watu wa kazi.

MASHABIKI wa Yanga hawaiamini timu yao na hata timu pinzani zinakiona kikosi hicho hakina mvuto, lakini winga mkongwe, Mrisho Ngassa, anaamini watawashangaza wengi na kuwanyamazisha.

Ngassa ameliambia Mwanaspoti kwamba hakutaka kuzungumza awali kwani alitaka kujiridhisha na amebaini kuwa timu yao ina kikosi cha maana chenye watu wa kazi.

Alisema msimu ujao timu ya itazipa shida timu nyingi pinzani kutokana na kuundwa na kikosi chenye watu wa kazi ambao anaamini wataleta mafanikio.

Winga huyo mkongwe alisema katika maandalizi yao mpaka walipofikia sasa, mbinu wanazopewa na makocha wao zimeongeza kasi na akili ya mpira.

Alisema anajua wengi hawaamini hilo, lakini mpaka kumalizika kwa mzunguko wa kwanza endapo mambo ya utawala na umoja yatadumishwa, basi wanaoibeza timu yao watanyamaza.

“Unajua mimi sikuwa nataka kuongea na vyombo vya habari tangu niliposaini, nilitaka kwanza nijiridhishe juu ya ubora wa timu, watu wanaongea, lakini hii timu itawanyamazisha,” alisema Ngassa.

“Nimeangalia wachezaji tuliosajiliwa na tuliowakuta, kwanza kikosi cha msimu ujao kitakuwa na tofauti kubwa, angalia mazoezi tunayoyapata kutoka kwa makoch.

“Ukiyachanganya hayo kwa pamoja nakuhakikishia wanaodhani kwamba Yanga ina timu mbovu watatuunga mkono kimyakimya na wasiotupenda watanyamaza, subirini mtaona.”