Mastaa watano Simba wapewa kazi maalumu

Muktasari:

  • Mastaa ambao, Aussems amewataja ni pamoja na Muivory Coast Pascal Wawa, Emmanuel Okwi raia wa Uganda, Mnyarwanda Meddie Kagere, Mzambia Cletus Chama na Erasto Nyoni.

Dar es Salaam. Ujanja aliofanya Kocha Mkuu wa Simba, Patrick Aussems ni kuwaandaa mastaa wake watano kwa ajili ya mechi yao ijayo ya Ligi Kuu Bara dhidi ya Ndanda FC.

Mastaa ambao, Aussems amewataja ni pamoja na Muivory Coast Pascal Wawa, Emmanuel Okwi raia wa Uganda, Mnyarwanda Meddie Kagere, Mzambia Cletus Chama na Erasto Nyoni.

Amesema, amefanya maamuzi hayo kwa sababu anaamini mchezo utakuwa mgumu kwao.

"Kila kocha ana mipango yake, nimewaacha wachezaji hao watano kwa ajili mchezo wa wiki ijayo, kwetu ni mgumu na tunahitaji ushindi kwa namna yote," alisema Aussems.

Amesema, lengo la kuwaandaa hao ni mipango tu ingawa wachezaji wote alionao kwenye timu na kundi zima kwa ujumla kila mmoja ana msaada wake.

"Wapo wachezaji ambao wamekuwa wanacheza dakika zote 90, lakini wapo wengine wanacheza chini ya hizo si kwamba hawana msaada, wote ni sawa isipokuwa ni katika mbinu na malengo ya kutafuta mafanikio,"alisisitiza Aussems ambaye ni Mbelgiji.

Mchezo wa Simba na Ndanda utacheza wiki ijayo Uwanja wa Nangwanda Sijaona, mkoani Mtwara.