Bandari yatibua rekodi ya Magereza

Muktasari:

Magereza ilikuwa na rekodi ya kutofungwa tangu kuanza kwa Ligi hiyo wiki iliyopita lakini jana ikaambulia kipigo cha magoli 38-23 kutoka kwa Bandari.

Dar es Salaam.Timu ya netiboli ya Bandari imetibua rekodi ya maafande wa Magereza katika mashindano ya netiboli ya Ligi daraja la pili inayofikia tamati leo kwenye viwanja vya JK Youth Park, Dar es Salaam.
Magereza ilikuwa na rekodi ya kutofungwa tangu kuanza kwa Ligi hiyo wiki iliyopita lakini jana ikaambulia kipigo cha magoli 38-23 kutoka kwa Bandari.
Katika mchezo huo ambao uliwavutia mamia ya mashabiki uwanjani hapo, Bandari ilianza kujihakikishia ushindi tangu kota ya kwanza kwa kutoruhusu kufungwa.
Mechi nyingine, Chemchem iliigaragaza Pamoja Youth kwa kuifunga magoli 75-18, Vingunguti ikichomoza na ushindi wa magoli 44-36 ya Polisi.
Ligi hiyo itafikia tamati leo kwa mchezo kati ya Bandari na Cocacola ambao utashuhudiwa na mgeni rasmi, mkuu wa Wilaya ya Ilala.