Liverpool yaitekenya West Ham 4-0

London, England. Mabao ya Mohamed Salah, Sadio Mane, Daniel Sturridge yameipa ushindi mnono klabu ya Liverpool kwenye mchezo wa Ligi Kuu England Uliopigwa leo Jumapili.

Mo Salah alifungua kalamu ya mabao kwa kuifungia timu yake bao la mepema dakika ya 20 kipindi cha kwanza, huku Mane akitupia wavuni mabao yake mawili katika mchezo huo.

Timu hizo ambazo ni kongwe  England, lakini mchezo uliwaelemea zaidi West Ham ambao walionekana kupoteana na kuzidiwa mbinu za uwanjani katika kusaka mabao.

West Ham hadi mwisho wa mchezo imejikuta ikipokea sapraizi ya mabao manne jambo ambalo limemfanya kocha Jurgen Klopp kuangusha tabasamu baada ya dakika 90 za mchezo kukamilika.

Msumari wa mwisho wa moto wa Sturridge uliwawezesha Liverpool kuondoka kifua mbele na kujisafishia njia mapema.

Hata hivyo, kocha wa timu hiyo amewataka wachezaji wake kucheza kwa bidii msimu huu ili kuhakikisha wanashinda kila mechi kisha kunyakua taji la msimu huu.