Lipuli yaitangazia vita Simba

Muktasari:

Timu hiyo ya Iringa inafundishwa na wachezaji wa zamani wa Simba, Amri Said na Selemani Matola

Iringa. Lipuli FC imesema itaingia uwanjani kwa lengo kuweka rekodi ya kuwa timu ya kwanza kuifunga Simba msimu huu wakati wataposhuka kwenye Uwanja wa Samora, Iringa Jumamosi hii.

Mchezo huo wa ligi awali ulikuwa uchezwe kesho Aprili 20, lakini kutokana na wammiliki wa uwanja kuwa na matumizi nao imesababisha mechi hiyo kusogezwa mbele hadi Aprili 21 Jumamosi umewaweka mashabiki wa timu zote mbili kuwa katika hali ya kuusubiri kwa hamu kubwa kufuatia matokeo ya mchezo wa awali kumalizika kwa sare 1-1 zilipokutana jijini Dar Es Salaam.

Akizungumza mchezo huo leo asubuhi, Kocha Msaidizi wa Lipuli Fc, Seleman Matola amesema maandalizi yote yamekamilika na kuahidi kuwafunga vinara hao wa ligi Simba Sc katika mchezo huo.

“Namshukuru Mwenyezi Mungu kikosi changu kiko salama maandalizi yamekuwa ni mazuri wachezaji wamejiandaa kwa ajili ya mchezo wa Jumamosi, samba ni timu kubwa timu ngumu timu ambayo imewekeza katika mpira ambayo imefanya vizuri katika msimu huu,” alisema Matola.

Matola aliongeza “Simba haijafungwa sisi tunataka tujiandae tuwe timu ya kwanza kumchinja mnyama katika uwanja wa nyumbani kwa hiyo maandalizi ya kupata pointi tatu yanaenda vizuri kabisa.”

Lipuli Fc kwa sasa ipo nafasi ya 8 katika msimamo wa ligi ikiwa na pointi 31, wakati Simba inaongoza Ligi Kuu ikiwa na pointi 58.