Kwa Kimenya imeshaanza kulipa mbona!

Muktasari:

  • Kimenya amesema, awali alikuwa anaona kama anapewa majukumu magumu na asiyoweza akaona kama anaonewa lakini kumbe yalikuwa maandalizi kwa ajili ya kuisaidia timu na wamefanikiwa.

 Dar es Salaam. Kiraka wa Tanzania Prisons, Salum Kimenya amesema anaanza kufurahia uamuzi wa Kocha Abdallah Mohammed 'Bares' kumchezesha kila namba katika kikosi chake kwa sababu matunda tayari ameshaanza kuyaona.

Kimenya amesema, awali alikuwa anaona kama anapewa majukumu magumu na asiyoweza akaona kama anaonewa lakini kumbe yalikuwa maandalizi kwa ajili ya kuisaidia timu na wamefanikiwa.

Amesema hadi sasa ana mabao manne aliyofunga akichezeshwa kama mshambuliaji, mawili ameyafunga katika mchezo wa ligi dhidi ya Mtibwa Sugar na mengine mawili kwenye mechi ya kirafiki dhidi ya Mbeya kwanza.

"Unajua mwanzo nilikuwa naona kama naumizwa napewa majukumu ambayo si yangu lakini sasa naona kabisa nanufaika, naweza kucheza nafasi yoyote na nikafanya vizuri mfano  ni katika safu ya ushambuliaji nimeweza kuwa msaada kwa timu kupata matokeo nikipangwa nafasi hiyo," alisema.

Kimenya aliongeza, kuelekea mchezo dhidi ya Ruvu Shooting anategemea kufanya makubwa zaidi katika nafasi yoyote atakayopangwa huku akiweka wazi kuwa safu mwalimu amebaini mapungufu katika safu yao ya ulinzi katika mchezo wao wa leo dhidi ya Mbeya kwanza atayafanyia kazi kabla ya kukutana na Ruvu Stootingi Jumamosi.

"Tulianza kuwafunga lakini hawakuonyeshja kukata tamaa walipambana na kusawazisha mabao yote mawili tatizo kubwa lililoonekana na kukosa umakini kwa mabeki wetu ambao waliluhusu washambuliaji wa timu pinzani kuingia eneo la hatari na kufanikiwa kusawazisha mabao yote mawili," alisema.