Fomu za kuongoza kikapu bei moto

Muktasari:

Ofisa Habari wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Najaha Bakari alisema  fomu zitaanza kutolewa keshokutwa Alhamisi katika ofisi za BMT, Dar es Salaam.

Dar es Salaam. Shirikisho la Mpira wa Kikapu Tanzania (TBF) limetangaza gharama za kuchukua fomu za kuwania uongozi ni  Sh 150,000 kwa Sh 100,000 katika uchaguzi utakaofanyika Desemba 30.
Ofisa Habari wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Najaha Bakari alisema  fomu zitaanza kutolewa keshokutwa Alhamisi katika ofisi za BMT, Dar es Salaam.
"Nafasi ya rais, makamu wa rais, katibu mkuu, katibu mkuu msaidizi na mweka hazina fomu zitatolewa kwa Sh 150,000 huku nafasi nyingine zote gharama ya fomu itakuwa Sh 100,000.
"Mwisho wa kuchukua fomu itakuwa Desemba 22 na baada ya hapo tutafanya usaili kabla ya kuelekea kwenye uchaguzi mkuu, kuhusu mkoa utakapofanyika tutautangaza baadae na sharti  mgombea awe Mtanzania," alisema Najaha.
Katika hatua nyingine, Najaha ameitaka mikoa ambayo bado haijathibitisha ushiriki wao kwenye mbio za JICA ambazo ni maalumu kwa ajili ya kuwaandaa wanariadha wanawake kushiriki Olimpiki ya 2020 wafanye hivyo kwani leo, Jumatano ndiyo mwisho.
"Mikoa 16 kati ya 31 iliyopo ndiyo imethibitisha kushiriki na Jumatano 'leo' ndiyo mwisho, hivyo niisisitize ile ambayo haijathibitisha kufanya hivyo kabla ya pazia kufungwa," alisema Najaha.