Kiiza anarudi kucheza Bongo

Muktasari:

Mshambuliaji huyo amecheza kwa mafanikio katika klabu za Yanga na Simba kabla ya kutimkia Afrika Kusini,  sasa Sudan.

Dar es Salaam. INASEMEKANA msimu ujao, mshambuliaji wa zamani wa Yanga na Simba, Hamis Kiiza ‘Diego’ anaweza akaonekana kwenye Ligi Kuu Bara, ingawa haijajulikana atavaa uzi wa timu gani.

Kiiza amekaririwa akisema anazungumza na timu mbalimbali za Bongo na kwamba kuna uwezekano mkubwa wa kurejea kucheza ligi ya Tanzania anayoifuatilia kwa ukaribu ili kujua kinachoendelea.

"Ligi ya Bongo ina ushindani wa hali ya juu, ninazungumza na timu mbalimbali ingawa siwezi kuziweka wazi kwa sasa, mambo yakienda sawa itajulikana naamini bado nitaonyesha uwezo wa hali ya juu, siri ni kujituma na kujitambua basi," alisema Mganda huyo.

Kiiza kwa sasa anacheza soka la kulipwa Sudan katika klabu ya Al-Hilal SC inayoshiriki Ligi Kuu ya nchini humo.