JKT Ruvu yaanzisha dozi kwa Ashanti uwanja wake mpya

Muktasari:

JKT Ruvu ambayo ilishuka daraja msimu uliopita imeonekana kupania kurejea tena kwa kishindo ligi kuu msimu ujao kutokana na kuana vizuri ligi daraja la kwanza.

Dar es Salaam. JKT Ruvu  imeichapa  Ashanati United  bao 1-0 katika mchezo wa Ligi Daraja la Kwanza uliofanyika jana Ijumaa jioni kwenye Uwanja wa Michael Joseph Isamuhyo uliopo Mbweni JKT.
JKT Ruvu ambayo ilishuka daraja msimu uliopita imeonekana kupania kurejea tena kwa kishindo ligi kuu msimu ujao kutokana na kuana vizuri ligi daraja la kwanza.
Bao la dakika ya 25 lililofungwa na Rahim Juma lilitosha kuipa ushindi timu hiyo   na hivyo kuongoza kundi A kwa kufikisha pointi sita.
Kabla ya ushindi dhidi ya Ashanti United, JKT Ruvu ilishinda pia mchezo wa kwanza  kwa kuwafunga ndugu zao Mgambo JKT ya Tanga mabao 2-0 .
Kocha wa kikosi hicho Bakari Shime amefurahia matokeo hayo na  ametamba kuwa wataendeleza moto wao mpaka wahakikishe wanarejea tena Ligi Kuu.
"Tunashukuru kupata ushindi katika mechi mbili ingawa hatutakiwi kubweteka kwani ligi ni ngumu kila timu inapambana lakini tumejipanga kuhakikisha tunafanya vizuri na kurejea tena kwenye ligi," alisema Shime.