Iwobi arejea Arsenal kuivaa Newcastle

Muktasari:

Nyota huyo wa Nigeria kwa sasa ameanza kujihakikishia namba katika kikosi cha kwanza cha Arsenal

London, England. Kocha wa Arsenal, Unai Emery amesema kesho atamuanzisha katika kikosi chake kitakachoikabilia Newcastle United, mshambuliaji kinda wa Nigeria, Alexander Iwobi.

Mshambuliaji huyo mwenye miaka 22 alikuwa mgonjwa hivyo kushindwa kuichezea Arsenal katika mchezo uliopita dhidi ya Cardiff City.

Pia, Iwobi alishindwa kuichezea Nigeria ‘Super Eagles’ dhidi ya Seychelles wiki iliyopita katika mchezo wa kufuzu fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika hapo zitakazopigwa mwakani nchini Cameroon.

Kocha Emery ametangaza leo kwamba ameridhishwa na kazi ya mchezaji huyo katika mazoezi aliyoyafanya na wenzake hivyo atamuanzisha hapo kesho dhidi ya Newcastle United.

Bila shaka kocha wa Arsenal anavutiwa na mbio za Iwobi akiamini zinaweza kusaidia kuwapa matokeo ambayo kwa sasa wanayahitaji sana baada ya kuanza vibaya Ligi ya msimu huu.