Hee! Eti Ufaransa wamelipa kisasi

Muktasari:

  • Deschamps alisema kuwa kufungwa na Ureno katika mchezo wa fainali za Euro katika dakika za nyongeza kuliwauma sana na sasa anaona kama ‘Les Bleus’ wamefanikiwa kujipooza kwa kuituliza Ubelgiji kwa bao 1-0 na kutinga fainali.

Moscow, Russia. Baada ya kuiongoza Ufaransa kutinga fainali ya Kombe la Dunia 2018, Kocha wa Ufaransa, Didier Deschamps, alisema anajina kama wamelipa kisasi cha kufungwa na Ureno kwenye fainali ya Euro 2016.

Deschamps alisema kuwa kufungwa na Ureno katika mchezo wa fainali za Euro katika dakika za nyongeza kuliwauma sana na sasa anaona kama ‘Les Bleus’ wamefanikiwa kujipooza kwa kuituliza Ubelgiji kwa bao 1-0 na kutinga fainali.

“Kila tulipokumbuka yaliyotutokea miaka miwili iliyopita kwa hakika tunaumia sana kwani tulipoteza mchezo mbele ya mashabiki wetu tunataka kuitumia nafasi hii kujifariji kwa kutwaa ubingwa,” alisema.

Alibainisha kuwa anawapongeza wachezaji wake kwa namna walivyojituma katika mchezo huo hadi kuibuka na ushindi wa bao 1-0, ambalo limewapeleka fainali ya michuano hiyo.

Wakizungumzia mchezo huo wachezaji karibu wote wa Ufaransa walisema sasa wanafikiria namna ya kupambana katika mchezo wa fainali ili historia ya miaka inayoishia na -8 iweze kujirudia wakisema akina Zinedine Zidane walitwaa ubingwa wa Dunia mwaka 1998 wanaamini na wao watatwaa mwaka huu 2018.