Hapatoshi Safaricom Kisii Half Marathon kesho

Nairobi, Kenya. Mabingwa mtetezi wa mbio za Safaricom Kisii Half Marathon, Philes Ongori na Joseph Koech, watakuwa na kibarua kigumu cha kutetea ubingwa wao katika makala ya 9 ya mbio hizo, zitakazofanyika kesho, mjini Kisii, Kenya.
Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa riadha, ukanda wa Nyanza Kusini, Peter Angwenyi ni kwamba Ongori na Koech watachuana na wafukuza upepo wengine 400, wakiwemo bingwa wa zamani Grace Momanyi, Teresa Omosa na mshindi wa Mully half Marathon, Sammy Nyokaye.
“Maandalizi yamekamilika, kuna wanariadha zaidi ya 400 waliojitokeza kupambana na Koech na Ongori. Mbio hizo kama mnavyofahamu zimekuwa zikifanyika kwa ufanisi mkubwa sana. Tunaamini mshindi atapatikana kwa haki," alisema Angwenyi.
Mshindi wa kwanza ataibuka na kitita cha shilingi 100,000, huku washindi wa pili wakiondoka na shilingi 50,000.